Kiongozi wa muungano wa Azimio La Umoja One Kenya Raila Odinga hii leo ameongoza wafuasi katika maandamano ya kuipinga serikali katika eneo la Imara Daima jijini Nairobi.

Odinga aliandamana na kinara mwenza wa Azimio Martha Karua, Kalonzo Musyoka wa Wiper Party pamoja na viongozi wengine wa upinzani.

Maandamano ya leo ni awamu ya tatu ya maandamano dhidi ya serikali.Suala la kutaka kushushwa kwa bei ya bidhaa muhimu lilisheheni maandamano ya leo.

Wakati uo huo ofisi za chama cha UDA huko Siaya zimevamiwa na kuteketezwa kwa moto na watu wanaokisiwa kuwa waandamanaji wa Azimio la Umoja.

Katika video zilizozikisambaa kwenye mtandao wa kijamii, jengo hilo lilionekana kuteketea kwa moto huku madirisha mengi yakivunjika.

Haya yanajiri wiki moja baada ya kundi la waandamanaji kuharibu ofisi za UDA mjini Kisumu.Waandamanaji hao walivamia eneo hilo na kupora bidhaa za thamani isiyojulikana na kuchoma gari la mmoja wa wafanyakazi wa ofisi hizo.

March 30, 2023