Muungano wa Azimio La Umoja One Kenya umetangaza kuwa utafanya maandamano dhidi ya serikali kwa siku tatu mfululizo wiki ijayo kuanzia Jumatano hadi Ijumaa.

Katika taarifa iliyotolewa siku ya Ijumaa, muungano huo ulisema kutokana na matakwa ya umma, umelazimika kubadili mpango wake wa awali wa kufanya maandamano siku ya Jumatano pekee.

Haya yanajiri licha ya onyo kali la serikali ambayo imeapa kutovumilia maandamano hayo ambayo yamesababisha vifo vya watu kadhaa, wengine wengi kujeruhiwa na mali ya thamani isiyojulikana kuharibiwa.

Siku ya Alhamisi, Rais William Ruto aliwakashifu mtangulizi wake Uhuru Kenyatta na kinara wa upinzani Raila Odinga kuhusu kile alichokitaja kuwa kuandaa machafuko nchini kwa kisingizio cha maandamano ya amani dhidi ya serikali.

Rais aliendelea kumshutumu Odinga kwa kujaribu kuhujumu serikali zote tatu zilizopita kwa maandamano.

July 14, 2023