BY ISAYA BURUGU 19TH JULY 2023-Usalama umeimarishwa katikati mwa jiji la Nairobi na maeneo yaliyo karibu huku mandamano yaliyoitishwa na mungano wa Azimio  kupinga gharama ya juu ya kimaisha yakirejelewa leo.Maafisa wa polisi wa kuzima ghasia wameonekana wakilinda doria katika Barabara nyingi jijini Nairobi huku shughuli chache mno zikionekana kuendelea.

Maduka mengi  yamesalia kufungwa huku  magari mengi ya uchukuzi wa umma pia yakiamua kukaa mbali.Katika eneo la Kibra vijana wameonekana wakikusanyika na kuwasha magurudumu katika baadhi ya Barabara za kuingia na kutoka eneo hilo.

Hali imesalia kuwa tete.Hali kama hiyo imeshuhudiwa katika eneo la kupakia magari jijini Kisumu ambapo makundi ya watu wengi wao vijana wanaonekana wakijikusanya kwenye vikundi.

Katika miji ya Nakuru,Kisii,Mombasa,Nanyuki na Homabay maafisa wa polisi wamekita kambi kote wakidumisha usalama.Hadi wakati tukienda hewani shughuli chache zilikuwa zinaendelea katika miji husika huku watu wengi wakisalia manyumbani.Kule Kisumu wakaazi wanasema ni sharti serikali itafute mbinu ya kushughulikia  gharama ya juu ya kimaisha.

.Wakati hayo yakiarifiwa watu wawili wamekamatwa katika mtaa wa Mathare katika mandamano ya upinzani.Maafisa wa polisi wamekabiliana na  vijana waliokuwa wakindamana na kuwasha moto katika sehemu mbali mbali za mtaa huo.Maafisa wa polisi wanazidi kushika doria katika eneo hilo kama ilivyo kwenye sehemu zingine nchini.

 

July 19, 2023