Odinga Ushuru Tax

Kinara wa Azimio Raila Odinga hii leo amezuru hospitali ya Kenyatta kuwatembelea majeruhi waliolazwa katika hopsitali hiyo kutokana na mashambulizi katika mandamano yaliyopita.

Zaidi ya watu 20 wamelezwa katika hospitali hiyo sawa na hospitali zingine jijini Nairobi.

Odinga amelaani kile alichokitaja kama ukiukaji mkubwa wa kisheria kwa maafisa wa polisi anaosema waliwashambulia waandamanji wasiokuwa na hatia wala kujihami.

Ameitisha uchunguzi wa kina na kuwachukulia hatua maafisa husika. wakati huohuo viongozi kutoka eneo la Nyanza waliungana na wakaazi kufanya maombolezi ya watu waliouawa wakati wa maandamano hayo ya wiki jana.

Katika Kaunti ya Homa Bay, Gavana Gladys Wanga aliongoza viongozi na wafuasi wa Azimio kuwasha mishumaa kuwakumbuka waathiriwa wa maandamano.

Wanga na viongozi wengine wa eneo hilo waliokuwa wakizungumza wakati wa hafla hiyo katika Kisiwa cha Rusinga, eneo bunge la Suba Kaskazini walilaani ukatili wa polisi, ambao uliwaacha Wakenya wengine wakiwa wamekufa, na wengine kuuguza majeraha ya risasi.

Katika Kaunti ya Migori hali ilikuwa sawia ambapo wakaazi waliungana na Wakenya wengine katika maombolezi hayo, wakiongozwa na viongozi wa chama cha ODM kutoka eneo hilo.

Walifanya vikao vifupi vya maombi katika uwanja wa Posta, ambapo katibu mkuu wa chama cha ODM Joseph Olala aliwataka polisi kukoma kuwaua watu wasio na hatia wakati wa maandamano.

July 26, 2023