Waziri wa Usalama wa ndani Kithure Kindiki, amezitaka asasi za usalama kuwachukulia hatua za kisheria wabunge watatu wanaotuhumiwa kwa kufadhili mashambulizi katika kaunti ya Baringo.

Akizungumza alipozuru kaunti ya Baringo ili kutathmini hali ya usalama eneo hilo wakati mitihani ya kitaifa ya KCPE na KPSEA, Kindiki amesema kuwa serikali haitawavumilia watu wanaowafadhili wahalifu hao licha ya nafasi yao katika jamii.

Haya yanajiri wakati kukiendelea kushuhudiwa visa vya wizi wa mifugo na mashambulizi dhidi ya raia wasio na hatia yanayofanywa na wahalifu wenye silaha katika kaunti ya Baringo.

Zaidi ya maafisa 60,000 wa usalama wametumwa katika maeneo mbalimbali ya taifa ili kusaidia katika kudumisha usalama katika kipindi cha mtihani kuanzia hapo jana. Wakati huo huo maafisa wa DCI kaunti ya Nakuru hii leo waliwahoji wabunge watatu kwa tuhuma za kuchochea uhalifu kaskazini mwa bonde la ufa.

Kupitia wakili wao, watatu hao William Kamket, Julius Murgor na Peter Lochakapong wamesema kuwa kukamatwa kwao na kuhojiwa kuhusiana na mashambulizi hayo ni kinyume cha haki huku wakitoa wito kwa rais William Ruto kufanya mkutano nao ili waweze kutafuta suluhu ya kumaliza mashambulizi ya mara kwa mara katika kaunti ya Baringo.

October 31, 2023