Viongozi mbalimbali kutoka pembe zote za taifa hii leo wameongoza zoezi la upanzi wa miti, ambalo limeendeshwa katika sehemu mbalimbali nchini. Viongozi wakuu serikalini wakiongozwa na Rais William Ruto na mawaziri wote nchini wamepanda miti katika kaunti mbalimbali huku wakimpongeza rais Ruto kwa kubuni siku hii kwani itasaidia katika kuafikia lengo la miti 15b ifikapo mwaka 2032.

Hata hivyo shuguli hii pia ilitekelezwa na wasimamizi wa mitihani ambapo walipanda miti katika vituo vya mitihani wanavyosimamia kabla ya mtihani wa leo kung’oa nanga.

Katika kaunti hii ya Narok Gavana Patrick Ntutu ameongoza zoezi la upanzi wa zaidi ya miti 48,000 katika msitu wa Enoosupukia eneobunge la Narok Mashariki. Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Ntutu amesema kuwa zoezi la upanzi wa miti litaendelea hapa Narok hata baada ya siku hii huku akiwahimiza wakaazi wa kaunti hii kupanda miti katika boma zao ili kuongezea kiwango cha msitu hapa Narok.

Kauli ya Gavana Ntutu imeungwa mkono na katibu katika wizara ya viwanda na biashara Abubakar Hassan ambaye amesema kuwa uwepo wa miti utazuia ukame kwa kuvutia mvua.

November 13, 2023