Rais William Ruto amewahakikishia wakenya kuwa nchi itasitisha uagizaji wa chakula kutoka nje katika muda wa miaka 10 ijayo.

Rais, ambaye alizungumza alipokuwa akiweka jiwe la msingi la Mradi wa Nyumba za bei nafuu huko Nanyuki, alisisitiza haja ya taifa kujitegemea katika uzalishaji wa chakula katika jitihada za kuokoa gharama ya uagizaji.

Alisema nchi kwa sasa inatumia takriban Ksh.500 bilioni kuagiza chakula kutoka nje kila mwaka, akisema kuwa serikali yake inajitahidi kuimarisha uzalishaji ili kutegemea kikamilifu uwezo wa uzalishaji wa kilimo nchini.

Aidha ameongeza kuwa ataendelea kupambana na madalali wanaoagiza maziwa kutoka nje ya nchi na kuwaharibia soko wakulima wa maziwa wa humu nchini.

January 10, 2024