Rais Ruto akutana na Waziri Mkuu wa Japan Fumio Kishida

Taifa la Kenya limevuna pakubwa kufuatia ziara ya rais William Ruto, katika taifa la Japan, ambapo mataifa haya mawili yamesaini makubaliano ya kifedha yenye thamani ya shilingi bilioni 350.

Rais Ruto na Waziri Mkuu wa Japan Fumio Kushida katika kikao cha pamoja na waandishi wa habari mjini Tokyo, walithibitisha makubaliano haya ambayo yanalenga kuboresha uchumi na ustawi wa Kenya. Viongozi hao wawili walishuhudia utiaji saini wa makubaliano haya siku ya Alhamisi baada ya kikao cha mazungumzo.

SOMA PIA: Rais Ruto na Naibu Wake Waikosoa Mahakama kwa Kusimamisha Maendeleo.

Mojawapo ya vipengele muhimu vya makubaliano haya ni msaada wa shilingi bilioni 40 kwa njia ya Bondi, utakaosaidia katika kufadhili miradi ya miundombinu, haswa katika sekta ya nishati. Kando na msaada wa kifedha, mikataba mingine muhimu iliyoafikiwa na viongozi hawa wawili inajumuisha ushirikiano katika sekta ya Teknolojia, Habari na Mawasiliano (ICT), afya, fedha, na usalama.

Baadhi ya miradi itakayonufaika ni pamoja na Mfumo wa Miundombinu wa Dongo Kundu na Daraja la Mombasa Gateway katika ukanda wa Pwani, ambayo imepangiwa kupata mgao wa shilingi bilioni 260. Aidha Kenya imehakikishiwa msaada wa shilingi bilioni 30 kutoka Benki ya Ushirikiano wa Kimataifa ya Japan, ili kununua mashine zitakazotumika katika ununuzi wa mashine na bidhaa zingine za utendakazi.

February 8, 2024