Spika wa bunge la kitaifa Moses Wetang’ula amekiri kupokea hoja ya kumbandua mamlakani naibu wa rais Rigathi Gachagua iliyowasilishwa bungeni na mbunge wa Kibwezi Magharibi Mwengi Mutuse.

Wetang’ula alithibitisha kuwa baada ya kuichunguza, hoja hiyo inakidhi matakwa yanayohusiana na fomu na kiwango kilichoainishwa katika Ibara ya 145 (1) na 150 (1)b ya katiba na kanuni za kudumu za bunge ibara ya 64 (1).

Kwa upande wake, mbunge Mwengi ameelezea baadhi ya mashtaka yanayomkabili naibu wa rais, hatua iliyompelekea kuwasilisha hoja hiyo ya kubanduliwa kwake.

Wakati huohuo, Wabunge wameonywa dhidi ya kuzungumzia hoja ya kubanduliwa kwa naibu wa rais katika mikutano ya hadhara au mahojiano na waandishi wa habari.

Kiongozi wa wengi katika bunge la kitaifa Kimani Ichung’wa ameeleza kuwa itakuwa kinyume cha sheria iwapo mbunge yeyote amezungumzia suala hilo.

Aidha amesema kuwa baada ya kukamilika kwa mchakato wa kujadili hoja hiyo, wabunge wako na uhuru wa kuizungumzia.

October 1, 2024