Waziri wa Usalama wa Ndani Kithure Kindiki ametoa amri ya kuwaua wahalifu wowote wanaolenga maafisa wa usalama au kambi za usalama.

Akizungumza alipokuwa akizindua kambi ya GSU katika Eneo Bunge la Tiaty, Kaunti ya Baringo, Kindiki alisema mhalifu yeyote atakaye mpiga risasi afisa wa usalama atachukuliwa hatua kali.

Waziri huyo pia alisisitiza nia ya serikali katika kumaliza ukosefu wa usalama katika eneo hilo, na kuongeza kuwa serikali itaweka kambi kadhaa huko Tiaty ili kukomesha ujambazi unaoendelea katika eneo hilo.

Mbunge wa Tiaty William Kamket kwa upande wake alikaribisha kuanzishwa kwa kambi ya GSU na kuitaka serikali kutenga vitengo zaidi vya usimamizi ili kurejesha maeneo ambayo majambazi wamechukua kama makazi yao.

Aidha Kamket alitoa wito wa kutumwa kwa Askari wa Kitaifa wa Polisi wa Akiba ili kuwasaidia maafisa wa GSU kwa kuwasaka majambazi ambao bado wanatawala eneo hilo na kusababisha maafa.

September 22, 2023