Chama cha ODM kimeibua wasiwasi kuhusu mpango wa kutumwa kwa maafisa wa polisi wa Kenya kuongoza ujumbe wa Multinational Security Support (MSS) nchini Haiti.

Katika taarifa iliyotiwa saini na Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna, chama hicho kinataka serikali kuangazia upya uamuzi huo, na kuongeza kuwa mpango huo hauna thamani ya kimkakati kwa Kenya.

Chama hicho kilibainisha zaidi kwamba uingiliaji kati wa hapo awali nchini Haiti ulifanywa na baadhi ya mataifa yenye nguvu zaidi duniani, na kusababisha matokeo mabaya kwa kila tukio.

ODM pia iliwataka wabunge kutoidhinisha mpango huo utakapofikishwa bungeni.Siku ya Jumatatu, Mahakama Kuu ilizuia kwa muda kutumwa kwa maafisa hao nchini Haiti hadi pale kesi iliyowasilishwa mahakamani kupinga uamuzi huo itakaposikilizwa na kuamuliwa.

October 12, 2023