UMEME

Waziri wa Uchukuzi nchini Kipchumba Murkomen, sasa anasema kwamba huenda kuna mipango ya makusudi ya kuhitilafiana na mitambo ya nguvu za umeme katika uwanja wa ndege wa JKIA jijini Nairobi.

Kulingana chapisho kwenye ukurasa wake wa X, Waziri huyo amesema kwamba hulka ya kupotea kwa nguvu za umeme hata ingawa kuna mitambo ya jenereta ni ya kutamausha.

Murkomen amewataka maafisa wa polisi kuchukua hatua za haraka kuanzisha uchunguzi wa kina kuhusu tukio la hivi karibuni ambapo mitambo ya jenereta katika JKIA ilifeli kufanya kazi baada ya hitilafu ya nguvu za umeme, jambo lililosababisha giza kubwa sehemu kadhaa za uwanja huo. Hitilafu hiyo ya umeme ilitokea jana jioni wakati nchi nzima ilikumbwa na matatizo ya nguvu za umeme.

Aidha, Waziri huyo ameitaka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini Kenya (KAA) kushirikiana na wadau wengine wa usafiri na nishati kuhakikisha kwamba suluhisho la haraka linapatikana ili kuzuia matukio kama haya kutokea tena.

 

December 11, 2023