kamati ya mazungumzo

Bunge la taifa limeongeza muda wa kuhudumu wa Kamati ya Kitaifa ya Mazungumzo ya Pande Mbili kwa siku 30 zaidi. Kamati hiyo inayoongozwa na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Taifa, Kimani Ichungwa, na Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka, itaendelea na majadiliano yao kwa siku zingine 30, kuanzia tarehe 28 ya mwezi huu.

Awali, kamati hiyo ilipewa muda wa siku 60 kukamilisha mazungumzo yao kabla ya kuwasilisha ripoti yao ya mwisho, ila sasa muda huo umeongezwa baada ya wanachama kupendekeza kuongezewa muda zaidi.

Lengo la mazungumzo hayo ni kuafikia makubaliano ambayo yatawezesha kuleta suluhisho la kisiasa na kuleta umoja nchini. Ripoti ya mwisho inatarajiwa kuwasilishwa kwa Rais William Ruto na Kiongozi wa Upinzani Raila Odinga kufikia tarehe 26 mwezi ujao.

October 17, 2023