Mpiganiaji uhuru Marehemu Mukami Kimathi amezikwa nyumbani kwake huko Njabini, Kaunti ya Nyandarua.

Familia na marafiki pamoja na viongozi wa ngazi ya juu serikalini walikongamana ili kutoa heshima za mwisho kwa mama Mukami.

Jamaa zake wamemmiminia sifa tele na kumataja kama mama aliyejitolea kupigania uhuru na umoja wa Kenya huku wakisema kuwa alisimamia haki na ukweli.

Mama Mukami alifariki tarehe 4 mwezi huu wa mei akiwa na umri wa miaka 101. Alifariki alipokuwa akipokea matibabu katika hospitali moja jijini Nairobi baada ya kupata matatizo ya kupumua.

Hayati Mukami atakumbukwa sana kwa mchango wake wakati wa harakati za kupigania uhuru wa Kenya. Alikuwa miongoni mwa wanawake shujaa waliokuwa wakiwapelekea chakula wapiganaji wa Mau Mau wakiwa msituni wakati vita vya ukombozi wa taifa hili kutoka mikononi mwa wakoloni vilikuwa vimechacha.

 

May 13, 2023