Washukiwa hao wanatuhumiwa kuhusika na vifo vya watu 429 katika eneo la Shakahola.

Mshukiwa mkuu wa vifo vya halaiki eneo la Shakahola, Paul Nthege Mackenzie, pamoja na washukiwa wengine 94, wamekana mashtaka tano yanayowakabili baada ya kufikishwa mahakamani siku ya Alhamisi. Mashtaka hayo ni pamoja na kujihusisha na uhalifu wa kupangwa, kutoa mafunzo ya itikadi kali, na kusaidia katika vitendo vya ugaidi.

Washukiwa hao ambao wanahusishwa na kanisa la Good News International linaloongozwa na Mackenzie, wanatuhumiwa kuhusika na vifo vya watu 429 katika eneo la Shakahola kati ya mwaka 2020 na 2023. Aidha walikanusha mashtaka yote yaliyowasilishwa mbele ya Mahakama ya Shanzu.

SOMA PIA: Mhubiri Ezekiel Odero afika mbele ya kamati ya seneti inayochunguza mauaji ya shakahola.

Mashtaka hayo pia yanadai kwamba washukiwa hao walihusika katika kitendo cha ugaidi kwa kuwasafirisha wanachama na wafuasi wa kanisa la Good News  kati ya Shakahola na Malindi mjini, hivyo kuhatarisha maisha yao. Pia, wanadaiwa kupatikana na nyaraka zinazohusiana na makosa ya kigaidi  kwa mujibu wa Sheria ya Kuzuia Ugaidi ya mwaka 2012.

Upande wa mashtaka uliwasilisha ombi la kupinga kuachiliwa kwa dhamana kwa washukiwa hao, na uamuzi utafanyika tarehe nane mwezi kesho.

 

January 18, 2024