Mfalme Charles Kuzuru KENYA

Rais William Ruto alikuwa mwenyeji wa Kamishna Mkuu wa Uingereza, Neil Wigan, leo katika Ikulu ya Nairobi, katika jitihada za maandalizi ya ziara ya Mfalme Charles III na Malkia Camilla nchini Kenya. Ziara hiyo inatarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 31 mwezi huu wa Oktoba hadi tarehe 3 mwezi Novemba.

Baada ya kikao hicho, Rais Ruto alieleza imani yake kwamba ziara ya Mfalme Charles, itakayokuwa ya kwanza tangu kutawazwa kwake mwezi Mei mwaka huu, itakuwa na manufaa makubwa kwa Kenya. Alisisitiza kuwa ziara hii itachangia kuboresha mahusiano kati ya Kenya na Uingereza, na kuimarisha ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

SOMA PIA: Rais Ruto kuhudhuria hafla ya Kutawazwa kwa Mfalme Charles III

Ziara ya Mfalme Charles na Malkia Camilla itahusisha maeneo kadhaa, ikiwa ni pamoja na kaunti za Nairobi na Mombasa, na inaonekana kama hatua muhimu katika kuendeleza ushirikiano wa kidiplomasia na biashara kati ya nchi hizi mbili. Mkuu wa baraza la Mawaziri Musalia Mudavadi ambaye pia anahusika katika mahusiano ya nje pia alihudhuria kikao hicho.

 

October 23, 2023