BY ISAYA BURUGU 19TH MAY 2023-Rais William Ruto amemteua aliyekuwa Waziri wa Michezo Rashid Echesa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya kitaifa ya Chemichemi za maji  .Kwa mujibu wa notisi ya gazeti la serikali ya Mei 19, 2023, Echesa itahudumu kwa muda wa miaka mitatu, kuanzia tarehe 19 Mei 2023.

Itakumbukwa kwamba Echesa alihudumu kama waziri wa michezo katika serikali ya rais Mustaafu Uhuru Kenyatta, lakini alitimuliwa kutokana na madai ya utepetevu na ubadhirifu wa fedha katika wizara yake  mwaka 2019.

Echesa alikabiliwa na sakata kadhaa wakati wa utawala wa rais mustaafu Uhuru Kenyatta.

Disemba 2021, mahakama ya Nairobi ilimuachilia huru katika kesi ya  kashfa ya silaha feki yenye thamani ya shilingi bilioni 39.

Hakimu Mkuu Mwandamizi Kenneth Cheruiyot alimwachilia kwa misingi kwamba mkurugenzi wa mashtaka ya umma alikosa kuwasilisha mashahidi muhimu katika kesi hiyo.

Cheruyoit aliamua kuwa hakuna ushahidi wa kuwaweka washtakiwa katika utetezi wao. Echesa alikuwa ameshtakiwa kwa kupanga njama ya kutenda uhalifu, Kupata pesa kwa njia ya udanganyifu.

May 19, 2023