Serikali ya kaunti ya Narok imezindua kituo cha dharura ya kukabiliana majanga mjini Narok. Kituo hiki kimeanzishwa kwa lengo la kuwasaidia wale wanaokumbwa na mikasa mbalimbali na pia kusaidia kuzuia mikasa hii.

Akiongoza shughuli ya uzinduzi wa kituo hicho, gavana wa Narok Patrick Ntutu amesema hii ni hatua muhimu katika kuyakabili majanga kama vile mafuriko ambayo yamekuwa sugu katika miaka ya hapo awali kwenye kaunti hii na hasa Narok Mjini.

Kwa upande wake kamishana wa kaunti ya Narok Isaac Masinde amewataka wakazi wa Narok kuchukua tahadhari huku mvua ya El-nino ikitarajiwa kuanza hivi karibuni.

Masinde akizungumza wakati wa uzinduzi wa kituo cha kukabiliana na majanga amesema kuna maeneo hapa Narok ambayo tayari yameanza kushuhudia mvua kubwa ambayo imesababisha mafuriko. Aidha amewahimiza wakaazi kushirikiana na maafisa wa usalama katika kuripoti majanga yanapotokea.

October 10, 2023