Tume ya Kuajiri Walimu nchini TSC imewaagiza maafisa wote wa nyanjani ambao wako likizoni kurejea kazini tarehe 16 mwezi Oktoba 2023, kabla ya mitihani ya kitaifa kung’oa nanga.

Afisa mkuu Mtendaji wa TSC Nancy Macharia alisema hatua hiyo inalenga kuhakikisha awamu ya mwisho ya maandalizi ya mitihani ya kitaifa inafaulu.

Alikuwa akizungumza wakati wa uzinduzi wa msimu wa mitihani ya kitaifa 2023 katika makao makuu ya KNEC jijini Nairobi. Zaidi ya watahiniwa milioni 3.5 watafanya mitihani ya kitaifa mwaka huu, ikijumuisha mitihani ya KPSEA, KCPE, na KCSE.

Mwaka huu umetoa idadi kubwa zaidi ya watahiniwa wa KCPE kuwahi kusajiliwa nchini. Kulingana na Macharia, TSC imekagua jumla ya walimu 223,223 ambao watahudumu kama wasimamizi na wakaguzi. Wengine 37,731 watachukua nafasi ya watahini wa mitihani ya kitaifa ya 2023.

 

September 25, 2023