Wabunge wajadili mauaji ya wanawake

Wabunge katika bunge la kitaifa alasiri ya leo walijadili suala la mauaji ya wanawake ambalo limekuwa likigonga vichwa vya habari kwa majuma kadhaa sasa.

Viongozi hao wameeleza kutamaushwa na ongezeko la mauaji haya na kutoa mapendekezo ya kuweka sheria kali zaidi kwa washukiwa na watu wanaopatikana na hatia ya kutekeleza mauaji ya aina hii.

Mswada huu uliwasilishwa bungeni na mbunge mwakilishi wa kike wa kaunti ya Nairobi Esther Passaris. Katika mswada huo, Passaris aliitaka Wizara ya Usalama wa Ndani kuweka wazi taarifa kuhusu mauaji ya wanawake nchini, pamoja na hatua zilizochukuliwa katika uchunguzi wake. Aidha, alitoa wito wa kudumisha heshima kwa wahanga, hasa katika suala la uchapishaji wa picha kwenye mitandao na vyombo vya habari.

Mbunge Passaris pia alimtolea wito kiongozi wa taifa kutangaza mauaji ya wanawake kama janga la kitaifa na kutoa tamko la kupinga na kulaani visa vya aina hii.

SOMA PIA: Joseph Irungu maarufu Jowie apatikana na hatia ya kumuua Monica Kimani.

Idara ya Mahakama haikusazwa katika mdahalo huo, ikielekezewa kidole cha lawama kwa kuwaachilia kwa dhamana washukiwa wa mauaji. Wabunge wamependekeza kuimarishwa kwa mfumo wa haki, na kuitaka serikali kuvunja kimya kuhusu suala hili.

February 14, 2024