Wajumbe wa serikali na upinzani walikutana hii leo jijini Nairobi katika juhudi za kupanga ratiba ya mazungumzo.

Mkutano huo ulifuatia agizo la spika wa bunge la kitaifa Moses Wetangula aliyewataka viongozi wa Azimio na Kenya Kwanza kupanga Ajenda.

Uongozi wa bunge kutoka  miungano ya Azimio la Umoja na  Kenya Kwanza uliamua kuwachagua wabunge wa  Rarieda Otiende Amolo na mwenzake wa  Tharaka  George Murugara kuongoza mazungumzo baina ya pande hizo mbili.

Wabunge hao wawili wataongoza kundi linalojumuisha seneta Ledama Ole Kina, Edwin Sifuna, Enoch Wambua,  Amina Mnyanzi, Millie Odhiambo, mbunge David Pkosing (Azimio) na seneta  Boni Khalwale.

Wengine ni pamoja na Hillary Sigei, Esther Okenyuri, Mwengi Mutuse, Adan Keynan, Lydia Haika kutoka (Kenya Kwanza).

Aidha wakati wa mkutano wa leo, pande zote mbili  ziliibua wasiwasi  kuhusu orodha ya wabunge walioteuliwa kuwakilisha pande zote mbili huku Azimio ukipinga kuteuliwa kwa Adan Keynan (Jubilee party) kwenye kamati hiyo,Kenya kwanza  inapinga hatua ya Azimio kumteua David Pkosing (KUP) kama mwanachama  wa kamati hiyo.

April 20, 2023