BY ISAYA BURUGU,6TH NOV,2023-Waziri wa  Hazina ya Kitaifa Prof. Njuguna Ndung’u amepuuzilia mbali madai yaliyotolewa na Mdhibiti wa Bajeti Margaret Nyakang’o kuhusu jinsi Hazina ya Kitaifa inavyodaiwa kuzidisha bajeti ya mshahara wake kwa mara tatu na kwa nyongeza ya mishahara ya maafisa wengine wa Serikali.

Akizungumza mbele ya Kamati ya Kitaifa ya Majadiliano , Prof. Ndung’u alisema tayari amewasilisha suala hilo kwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu ili kubaini ukweli.Mdhibiti wa Bajeti, ambaye alifika mbele ya Kamati ya Kitaifa ya Mazungumzo Jumanne wiki iliyopita, alielezea kwa undani jinsi Hazina imekuwa ikibajeti kupita kiasi mishahara ya maafisa wakuu wa serikali kupitia Huduma za Mfuko Mkuu wa Serikali.

Hapo awali Hazina ilipanga bajeti ya mshahara wake wa kila mwaka kama Ksh.17.82 milioni, jambo ambalo lilisababisha afisi yake kuibua wasiwasi kwani kiasi hicho kilikuwa juu zaidi ya kile alichokuwa akipeleka nyumbani kila mwaka.

Hazina ingepunguza tu kiasi hicho hadi Ksh.10.15 milioni ambacho kilikuwa kikubwa zaidi ya mshahara wake wa kila mwaka wa Ksh.9.18 milioni.

Hazina pia iliweka bajeti ya Ksh.42.4 milioni kama mishahara na marupurupu ya Rais na naibu wake ilhali mishahara yao iliyotangazwa kwenye gazeti la serikali ni Ksh.32.05 milioni, tofauti ya Ksh.10.35 milioni.

Nyakang’o anasema alikuja kujua tatizo hilo kwa sababu lilimuathiri yeye binafsi na kwamba maafisa wengi wakuu wa serikali walioathirika hawajui tofauti hizo.

Anatoa wito wa ukaguzi wa haraka kuhusu suala hilo ili kuziba mwanya wa kile anachotaja kama ufisadi wa bajeti.

 

 

 

 

 

November 6, 2023